Friday, June 5, 2009

AKUFAAYE KWA DHIKI...WANAWAKE TUKOMBOANE

AKUFAAYE KWA DHIKI…. “WANAWAKE TUKOMBOANE”
By Shanande John

Helena, mwanamke mwenye ujauzito wa miezi mine, amekaa sebuleni, ndani ya nyumba nzuri ya kifahari, waliyonnunua na mumewe Samson, anawaza na kutafakari maisha ya ndoa yake yenye miezi mitatu tu, ilivyo na kila aina ya purukushani.

Anakumbuka enzi za urafiki wao, hadi uchumba, kabla hajaolewa akiwa tayari ana ujauzito wa mwezi mmoja. Ujauzito uliomlazimu Samson afunge naye ndoa. Sharti lililotoka kwa wazazi wa Helena. Maisha ya uchumba yalitojaa kila aina ya raha na starehe.

Samson alizoea kufika kwa Helena na kila aina ya zawadi. Alihakikisha jokofu ya Helena imejaa kila aina ya mboga, tunda na juisi. Nguo na viatu, na hata maua alipelekewa.

Kwa sasa, Helena anawaza hayo, kuwa mbona hayafanyiki tena, na ikiwa wapo pamoja, hizo huduma zinapelekwa wapi!! Na tena imekuwa siku hizi akidadisi jambo anapatiwa majibu ya mkato, hata kupigwa. Ni miezi mitatu tu katika ndoa.

Katika kuyawaza hayo, Helena anakumbuka rafiki yake Suzana. Anaamua kumpigia simu na kumwomba afike nyumbani kwake Helena mara moja.

Suzana anafanya hivyo, na kumkuta Helena sebuleni akiwa na huzuni kubwa sana. Suzana anadadisi “kulikoni?”

Helena anamweleza rafiki yake Suzana, maisha anayopitia na mumewe na kuhisi ana maisha mengine kwingine. Anamwomba Suzana amsaidie cha kufanya, kwa kuwa wamekuwa wakisaidiana tangu maisha ya chuoni, ambapo Helena aliweza Suzana malipo mbalimbali na ada.

Katika kulitafakari hilo, Helena anamhoji Suzana kama ataweza kujifanya mpenzi wa mumewe Samson, ili amrejeshee kwake, na awe kama walivyokuwa wanaishi kabla hawajaoana, kwa hali na mali. Wakapanga namna itakavyokuwa.

Suzana analitafakari hilo na kulikubali, na kumuahidi Helena kuwa hatamuangusha.
Huko nje, Suzana akawa anamvizia Samson, kama vile kumwomba lifti kuelekea sehemu tofauti tofauti, kwa kuwa aliishi karibu nao. Akawa anajifanya kumsema vibaya Helena, kwa mumewe Samson.

Samson akajikuta ana mahusiano ya karibu na Suzana, na kwenda naye sehemu mbalimbali za starehe. Suzana akaendelea “kumchafua” Helena mbele ya Samson, lakini anafanya kinafiki tu, kwani anapokutana na Helena, anamweleza kila kinachoendelea, japo pia Samson akiwakuta nyumbani, Suzana hujifanya kumdhalilisha Helena kuwa ni mwanamke mchafu na hafai kuwa mke wa mtu, ili mradi tu Samson asilkie hayo, kumfanya aone kuwa Suzana na Helena hawaivani kwa sasa.

Samson anaamua kumwagia Suzana hela lukuki. Anataka hata kumfukuza mkewe Helena nyumbani akidai nyumba inanunuliwa, na ameshapatikana mteja. Kumbe anataka kumpatia Suzana, naye Samson bila kujua kama Suzana anawasiliana hayo yote na Helena mkewe, tena anampatia na hizo fedha japo anazificha Samson asipopajua.

Wakati anafikiria na kupanga namna ya kuiuza nyumba, Samson akawa anafikia hotelini. siku moja Helena anaamua kwenda akijifanya kumtafuta siku nyingi, akiwa amembeba mwanae wa kike, aliyejifungua miezi mitatu iliyopita, mchafu mchafu, akimsihi mumewe arudi nyumbani wakalee mototo wao. Kumbe ni sanaa anamfanyia mumewe. Samson akajifanya hamtambui na kuamuru wahudumu wa hotelini wamfukuze.

Suzana na Helena wakatafuta nyumba nyingine ya kumhifadhi Helena kwa muda Fulani, pamoja na mototo.

Akiwa ndani ya nyumba ya Samson na Helena, siku moja Suzana anaamua kumwalika Samson, bila kumwandalia chakula wala kinywaji chochote. Samson anafika na kukaribishwa kiti ndani ya nyumba ya kifahari ambayo kwa sasa anamilikishwa Suzana.

Suzana anaamua “kumwondolea uvivu” Samson, kwa kuanza kumweleza nia na madhumuni ya wito huo, kuwa si kama amefanya yote hayo kwa nia ya kumdhalilisha rafiki yake Helena, bali ni kumsaidia. Angependa kuona ndoa yake Samson na Helena inaendelea na kukua vema.

Anamuelezea habari nzima tangu alipoitwa na Helena kumwelezea matatizo ya ndoa yake na hata leo hii. Suzana anagonga meza mara tatu kwa nguvu, kama walivyoashiriana na Helena kabla.

Helena akiwa amembeba mototo wao wa miezi saba, wamependeza sana, anaingia sebuleni akitokea chumba kimojawapo cha ndani, na uso wa tabasamu zito. Anamwendea mumewe na kumsihi asimame ili ampokee mototo wao. Akiwa katika hali ya mshituko na mshangao, bila kuamini na yanayotokea, na kama vile hajielewi, anasimama na kumpokea mototo.

Anamwangalia Suzana bila kujua afanye nini au aseme nini.
anasimama na kuwaaga akiwaacha ndani wawili na mwanao ambaye mama yake alikuwa hajampa jina, akimwita “Baby”. Helena anajikaza na kumsogelea mumewe huku anabubujikwa na machozi yaliyojaa “heri na shari” anamkumbatia na kumwambia “Nakupenda sana mume wangu”…MWISHO

3 comments:

  1. Wow Shanande! Story yako imenifurahisha sana....hasa maudhui yake, ujasiri wa Helena na 'uaminifu' wa Suzana... Ingawa sidhani kama inawezekana mke kumruhusu shoga yake awe na mahusiano ya mapenzi na mumewe kama mbinu ya kumrudisha mumewe kwake... well, I'm a man, can't be so sure of that. Now, what if the story ends up like Suzana betrays her friend by getting real and steals her husband forever...?

    ReplyDelete
  2. Shanande,
    Kisa chako kizuri! Umefanikiwa katika msuko wa kisa chenyewe, yaani mwanzo mtiririko na mwisho, baaas! Stori yako inakosa 'mtikisiko' ambao ndio nguzo kuu ya visa vifupi. Pamoja na kukosa mtikisiko, (yaani pale ambapo msomaji huchukuliwa hisia mzobemzobe, akajikuta analia au anasisimkwa au anaruka kutoka kitini au anahemkwa tu),pia tunakosa kuona hisia za wahusika wetu; hususan hili 'dude' Samson. Samson, ambaye anahusika na kisa chote kuliko mhusika mwingine yeyote, ambaye anaoneshwa kuwa chanzo cha visa na vitimbi, msongoa mambo, mharibifu, haoneshwi hisia zake. Yeye yuko tayari kuchukua mwanamke yeyote, wakati wowote, bila kupesa jicho.
    Haoneshwi kama binadamu mwenye hisia za kupenda, kubembeleza, kulizwa na mapenzi,... yaani unaweza kuhisi tu kuwa huyu ni 'mnyama' fulani!
    Ndiyo shida ninayoiona katika kisa hiki.
    Je, Helena ni malaika asiyekuwa na makosa walau kidogo? Naye anaoneshwa kuwa 'mzuri tu' au 'wa kuonewa tu'. Halafu huyu Suzana, anaendesha haya mambo yake kumsaidia Helena hadi kufikia kiwango gani na Samson? Wanafikia hatua ya kuwa 'wapenzi' wakati Suzana anamuekti huyu Samson au??? Nadhani nina maswali mengi mno, hivyo nadhani wenzangu watakuwa na maoni ya kunisaidia.
    Hatima: Kiini cha mafanikio ya visa vifupi ni hisia kali au za ndani na vitimbi, vurugu (ziwe za kimwili au za kihisia), na msuko bomba!
    Mwafrika Merinyo.

    ReplyDelete
  3. Michael Karani is my name. I'm a university student in UDSM majoring Linguistics and Literature.I would like to be a good writer. So please let me know from you, what assistance do you provide to young prospective writers and how can I join your club if any?
    Kind regards,
    Karani
    Mobile +255715826611

    ReplyDelete